Asasi za Kiraia nchini zimeshauriwa kuwa na mipango mikakati mizuri inayofungamana na mipango ya kitaifa ya maendeleo endelevu ili waweze kushiriki kikamilifu na kuchangia katika kujenga uchumi wa Taifa.

Katibu wa Baraza la Taifa la mashirika yasiyo ya kiserikali (NaCoNGO) Revocatus Sono ametoa shauri huu siku ya Jumatatu Oktoba 25, 2021 wakati akichangia mdahalo kuhusu mpango wa tatu wa maendeleo ikiwa ni sehemu ya sherehe za Wiki ya Azaki kwa mwaka huu zilizofanyika Mkoani Dodoma, Tanzania.

Pia Azaki zinatakiwa kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuweza kuwa na ushiriki mzuri wakati wa utekelezaji wa mipango na mikakati ya kitaifa ya maendeleo nchini,” alisema Sono.

Sono alifafanua zaidi ya kwamba changamoto kubwa iliyoko kwa sasa ni tabia ya Asasi za Kiraia nyingi nchini kufanya kazi bila kushirikiana, hali inayopelekea kukosekana kwa ushiriki wao wenye tija wakati wa utekelezaji wa mipango ya kitaifa ya maendeleo.

Hii imedhihirishwa wakati wa utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Maendeleo (FYDP III 2015/16 – 2020/21) ambapo ushiriki wa Azaki na Sekta Binafsi nchini unaelezwa kuwa sio wa kuridhisha na hivyo kusababisha mchango wao katika kuchangia ukuuaji wa uchumi wa Taifa kutoonekana.

Kwa sasa Tanzania inatekeleza mpango wa tatu wa maendeleo (FYDP III 2021/22 – 2025/26) uliozinduliwa mwaka huu ikiwa ni mwendelezo wa jitihada za Serikali kuboresha maisha ya wananchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi, ambapo Serikali imeeleza utayari wake wa kushirikiana na Azaki na Sekta Binafsi nchini wakati wa utekelezaji wa mpango huu.