Spika wa Bunge Job Ndugai amesema ofisi ya Bunge itaendelea kushirikiana na asasi za kiraia katika mazingira rafiki, huru, wazi, na sawa ili kuendelea kusukuma gurudumu la maendeleo ya Taifa huku akizitaka kurekebishana kwa zile zinazoenda tofauti.

Ndugai amesema hayo Oktoba 23, 2021 wakati akizungumza katika maonyesho ya wiki ya Azaki 2021 ambapo yeye alihudhuria kama Mgeni rasmi. Kauli mbiu ya mwaka huu ni Azaki na maendeleo.

“Natambua kwamba Bunge na Azaki ni wadau muhimu katika utendaji wa kazi hasa katika sera, sheria, bajeti, na masuala mbalimbali yanayowahusu wananchi, kuna mahali ambapo Serikali wakati mwingine haifiki lakini Azaki zinafika,” amesema Ndugai.

Hata hivyo amesema licha ya kazi kubwa inayofanywa na baadhi ya asasi za kiraia, zipo ambazo hazifanyi kazi vizuri ndiyo maana zilitungwa sheria mbalimbali za kudhibiti endapo mapengo yataonekana.